Tuesday, August 14, 2012

HANS POPE AIFUNGUKIA YANGA, MZAZI WA TWITE AHOFIA USALAMA WA MWANAE

Sakata la usajili wa Mbuyu Twite aliyejiunga Yanga, huku Simba nayo ikiingia naye mkataba, umeendelea kuwa 'kivutio', ambapo sasa Wekundu hao wa Msimbazi wameibuka na madai mapya.
Mwenyekiti wa Kamati ya usajili klabu ya Simba, Zacharia Hans Pope ameilaumu Yanga kwa kuuingiza mchezo wa soka kwenye machafuko.

Pope amesema kitendo cha wenzao kuwazunguka na kumshawishi Twite kurejesha fedha walizompa ili asajili Simba, kinaweza kuleta uhasama usio na ulazima."Tumepata taarifa kuwa baba mzazi wa Mbuyu (Twite) amemkataza mwanaye kuja kuichezea Yanga kwa hofu maisha yake."
"Mzee Twite anataka Simba na Yanga zikutane kufanya mazungumzo kwa lengo la kuweka mambo sawa kisha ndipo amruhusu kuja Tanzania," alisema Pope.
"Unadhani kwa kitendo walichofanya Yanga, mashabiki wa Simba watafurahi? Baba yake mzazi (Twite) amechukizwa na hali hiyo, anahofia usalama wa kijana wake," alisema Pope.
"Vita ya soka haina tofauti na ile ya siasa au dini. Kwa hiyo baba mzazi wa Mbuyu ameomba Yanga na Simba kumaliza suala hili mwanaye aweze kucheza soka kama ilivyo kazi yake."

Katika kusisitiza ukweli wa madai yao, Pope alisema tayari uongozi wa Yanga umeomba kukutana nao ili kuzunguza na kumaliza suala hilo.
"Ukweli ni kamba, hatuna tatizo na Yanga. Nafikiri siyo mara yao ya kwanza wala mwisho kutufanyia mchezo huu mchafu. Ni kawaida yao."

"Wameomba [Yanga] tukutane ili kumaliza utata wa suala hili, vinginevyo Twite hatakuja siyo kujiunga na Yanga au Simba, bali haji kabisa."
Aliongeza: "Tulianza mazungumzo na Bahanuzi (Said)wakatuzunguka na kumsainisha, ikawa hivyo tena kwa Kavumbagu (Didier) na sasa wametuma viongozi Kenya kutaka kumsainisha Pascal Ochien ambaye yupo na timu Arusha."

"Nafikiri Yanga kama wanataka kulipa kisasi cha mabao matano tuliyowafunga, wacheze mpira na siyo kutuzunguka na kusajili wachezaji wetu."
"Hata sisi tunaweza mchezo huo mchafu---ni kweli tunaweza kuwafanyia, lakini hatuoni sababu ya kufanya hivyo," alisema zaidi Pope.

Alipoulizwa mjumbe wa Kamati ya Utendaji na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Yanga, aliyefanikisha usajili wa Twite, Abdallah Bin Kleb, alikana kuwapo na makubaliano ya kukutana na Simba kuzungumza suala la mchezaji huyo.
Bin Kleb aliibeza kauli ya Pope na kusema inalenga kuwaziba mdomo mashabiki wa Simba ili wasahau kuzungumza suala la usajili wa Twite.

"Hakuna makubaliano ya sisi [Yanga] kukutana na Simba ili kuzungumza suala la Twite. Kwanza kwa nini tufanye hivyo wakati mchezaji tumemsajili kwa kufuata taratibu," alihoji Bin Kleb.
"Kama Simba wana matatizo na mchezaji ni wao, sisi hatuna matatizo na Twite wala mzazi wake, sasa iweje leo ashindwe kuja kujiunga na timu aliyopenda kuichezea?," alisema.

Alisema, Twite anatarajia kuja nchini wiki ijayo akitoka Kongo alikokwenda kuwasalimia wazazi wake ambao hakuonana nao muda mrefu.
Wakati huohuo, mshambuliaji mpya wa Simba George Ochan kutoka Kenya tayari ameshajiunga na wenzake, Arusha, huku Sihaune Abdulaziz kutoka Ghana akitarajia kutua leo.

MALIASILI KIMENUKA,MKURUGENZI WANYAMAPORI ATIMULIWA


Waziri wa Maliasili na Utalii Khamis Kagasheki

Mkurugenzi wa Wanyamapori katika Wizara ya Maliasili na Utalii, Obeid Mbangwa na wenzake wawili, wametimuliwa kazi kwa kashfa ya kutorosha wanyama hai 136 wa aina 14 tofauti kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia), usiku wa Novemba 26, 2010.


Mkurugenzi wa Wanyamapori alietimuliwa kazi Obeid Mbangwa

Hatua hiyo imefikiwa baada ya tume mbili zilizoundwa kuchunguza suala hilo bila kuhusisha wizara yenyewe, kumaliza kazi yake na kukabidhi ripoti kwa Waziri.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki alisema jana mjini Dodoma kuwa mbali na watuhumiwa hao, mtumishi mwingine wa wizara hiyo amevuliwa madaraka, wawili wamepewa onyo kali la maandishi na wawili uchunguzi dhidi yao unaendelea.

Mbangwa wakati wa kashfa hiyo ya kusafirisha wanyama hai wanaokadiriwa kuwa na thamani ya Sh170 milioni kwa ndege ya kijeshi ya Qatar, alikuwa Mkurugenzi Msaidizi Matumizi ya Wanyamapori.
Wengine waliotimuliwa kazi ni Simon Gwera na Frank Mremi waliokuwa Maofisa Uwindaji wa Kitalii, Cites na Utalii wa Picha mkoani Arusha.

Mkurugenzi Msaidizi, Uendelezaji Wanyamapori, Boneventura Midala amevuliwa madaraka kutokana na kutochukua hatua kikamilifu za ulinzi ambazo zingeweza kuzuia kutokea kwa utoroshaji wa wanyama. Wakati wa tukio hilo alikuwa Mkurugenzi Msaidizi, Sehemu ya Kuzuia Ujangili.

Katika hatua hizo, maofisa wanyamapori daraja la pili, wawili waliotekeleza maelekezo ya wakuu wao wa kazi yaliyo kinyume cha sheria wamepewa onyo kali la maandishi.

Kagasheki aliwataja maofisa hao kuwa ni Ofisa Leseni ya Uwindaji wa Kitalii, Cites na Utalii wa Picha Arusha, Martha Msemo na Ofisa Leseni Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii, Cites na Utalii wa Picha Dar es Salaam, Anthonia Anthony.

Rungu la wizara hiyo pia limemwangukia Mkuu wa Kituo cha Uwindaji wa Kitalii, Cites na Utalii wa Picha Arusha, Silvanus Ukudo aliyepewa onyo kali la maandishi kwa kushindwa kufuatilia kupata maelekezo ya Mkurugenzi wa Wanyamapori kuhusu mtumishi wake aliyekiuka sheria katika utoaji wa vibali.

Ukudo pia ameonywa kwa kushindwa kupeleka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, taarifa kuhusu mtumishi huyo ili achukuliwe hatua za kinidhamu.
Kagasheki alisema uchunguzi unaendelea dhidi ya watumishi wengine wawili, Ofisa Matumizi Endelevu ya Wanyamapori, Mohamed Madehele na Ofisa wa Kituo cha Uwindaji wa Kitalii, Cites na Utalii wa Picha Arusha, Mariam Nyallu.

Alisema kwa upande wa wafanyabiashara waliohusika katika kashfa hiyo, kesi inaendelea mahakamani na kwa upande wa Qatar, Serikali alisema: “Tumefanya kila jitihada. Tumewasiliana kupitia Makao Makuu ya Cites, Geneva, Uswisi, lakini Qatar pamoja na kukubali kupokea maombi yetu kutoka Cites, imekaa kimya.”

Kuhusu hatua zaidi dhidi ya watuhumiwa hao, Waziri Kagasheki alisema: “Kwa kuwa imebainika walihusika na vibali vilivyosababisha hao wafanyabiashara wakamatwe, suala hilo halijaishia hapo.”
Waziri huyo alisema atajitahidi kadri ya uwezo wake kusimamia wizara hiyo ili kuhakikisha sheria na taratibu zinafuatwa... “Sheria zipo nzuri, udhaifu mkubwa ni kwa watendaji wetu,” alisema.
Alipotakiwa kuzungumzia suala hilo Mbangwa alisema hajui chochote.

Alisema hadi jana alikuwa hana taarifa za kufukuzwa kazi hivyo hawezi kusema chochote hasa bila ushahidi.

Unasema wamenifukuza kazi, ndiyo wametangaza hivyo? Mimi sina taarifa hizo na hivyo siwezi kuelezea chochote,” aling'aka Mbangwa.