Friday, May 11, 2012

NYOSSO KUTIMKIA SAUZ


Juma Nyosso wa pili kulia waliosimama akiwa na kikosi cha Simba

Beki mashuhuri Juma Nyosso wa Simba, amepata soko baada ya Klabu ya Platinum Stars ya Afrika Kusini kutangaza kuwa inataka kumnunua kwa ajili ya msimu ujao.
Habari za uhakika kutoka ndani ya Simba zimeeleza kuwa uongozi wa timu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu ya Afrika Kusini (PSL), umeonyesha nia ya kumsajili Nyosso na ulifanya mazungumzo na Simba.
“Kweli jamaa wa Platinum Stars walikuja na kufanya mazungumzo. Wameonyesha wanamhitaji Nyosso,” kilieleza chanzo cha uhakika na kuongeza “ Mazungumzo yalifikia katika hatua nzuri kabisa lakini kuna mambo kadhaa ya kuangalia ndipo hilo likamilishwe.”
Mjumbe mwingine wa kamati ya usajili ya Simba aliliambia gazeti hili kuwa suala hilo lazima liidhinishwe na kamati ya usajili.
“Kamati ya usajili itamaliza kila kitu lakini itafanya hivyo baada ya kukutana na kocha Milovan ambaye ataeleza anachokitaka, pia ni wachezaji gani anataka wabaki, waondoke au waongezwe.

“Baada ya hapo tutaanza kufanya utaratibu, sasa inategemea huenda na Nyosso akaruhusiwa kuondoka,” alisema mjumbe huyo.
Platinum Stars inayofundishwa na Owen Da Gama ipo katika nafasi ya 10 katika PSL na kikosi chake kina wachezaji wote raia wa Afrika Kusini isipokuwa watatu, kipa Etame Soppo (Cameroon), Henrico Boates (Namibia) na Mohammed Chikoto (Niger).

Timu hiyo iliwahi kuripotiwa kumtaka Nyosso mwishoni mwa mwaka jana lakini baadaye viongozi wake walisita kuendelea na mazungumzo na Simba.

MASIKINI SAJUKI!! ZIMESALIA SIKU 2 KUELEKEA INDIA HALI YAZIDI KUWA MBAYA, WOLPER ATOA MIL 15


Sajuki akiwa kitandani na wasanii wenzake waliokwenda kumjulia hali

Masikini SAJUKI! Siku mbili kabla ya kwenda katika Hospitali ya Apollo nchini India kwa matibabu, afya ya stadi wa filamu za Kibongo, Sadick Juma Kilowoko ‘Sajuki’ ni ya kusikitisha ile mbaya.
Kadiri siku zinavyoyeyuka, hali ya Sajuki inazidi kuwatoa watu machozi baada ya kuzidiwa na kushindwa kunyanyuka kitandani. Laiti kama utamuona na ukashindwa kububujikwa na machozi basi utakuwa huna utu.



Wasanii wa Bongo movie wakiwa wamemzunguka Sajuki kitandani(Chini ya picha Wolper aliyetoa mil 15)

Tukio la kusikitisha lililowatoa machozi wasanii wenzake ni lile la Jumanne wiki hii nyumbani kwake Tabata Barakuda, Dar es Salaam ambapo msanii na prodyuza huyo wa filamu alishindwa kuamka kitandani kupokea dola elfu kumi (takribani Sh. milioni 15) alizozitoa mwigizaji mwenzake, Jacqueline Wolper kwa ajili ya matibabu huku akisindikizwa na mastaa wengine wa Bongo Movie.
Sajuki akiugulia maumivu huku akilalamika kujisikia vibaya, hivyo kuwaomba wasanii wenzake kwa heshima waingie chumbani kwake ili apokee fedha hizo.



Msanii wa Bongo movie akiwa ameshindwa kujizuia na kujikuta akimwaga chozi

Kitendo hicho ndicho kilichowafanya baadhi ya wasanii wenzake kushindwa kujizuia na kujikuta wakiangua vilio huku Sajuki akiwatuliza na kuwaomba wasilie wala wasihuzunike kwani kila kitu ni mapenzi ya Mungu.
“Msihuzunike ndugu zangu, naamini kila kitu ni mapenzi ya Mungu na si vinginevyo, jipeni moyo,” alisema Sajuki kwa tabu akiwa amelala kitandani akiwa amezungukwa na mastaa hao.

WOLPER Kwa upande wake Wolper aliyekuwa akimwaga machozi mithili ya bomba la mvua, alisema kuwa siyo kwamba ana fedha nyingi, ila ni namna alivyoguswa na mateso ya Sajuki.
“Siyo kwamba sina shida bali ni moyo wa kusaidia kuokoa uhai wa mwenzetu. Tulizoea kuwa naye location (sehemu ya kurekodia filamu) na kwenye tasnia yetu, anaumwa na hajiwezi, niliumia sana,” alisema Wolper aliyekuwa akifutwa machozi na wenzake.

WASTARA Naye mke wa Sajuki, Wastara Juma, huku akilia muda wote, alitoa shukurani zake za dhati kwa Wolper na kueleza jinsi alivyoguswa na kuona umuhimu wa kumsaidia mumewe
Habari kwa hisani ya Global Publishers.

NYOTA WA MAN UNITED AOMBA KUINOA SERENGETI BOYS


Quinton Fortune enzi zake akikipiga Man United

Mshambuliaji nyota wa zamani wa Manchester United, Quinton Fortune amefunguka kuwa yuko tayari kuifundisha timu ya Taifa ya Vijana ya Tanzania chini ya miaka 17 kama atapewa nafasi hiyo kwa sababu kiu yake ni kuona soka ya Kusini mwa jangwa la Sahara inakuwa na kufikia kiwango cha Afrika Magharibi na Kaskazini.


Quinton Fortune

Akizungumza na Mwananchi jana jijini Dar es Salaam, Fortune alisema ingawa haifahamu rekodi ya timu ya Taifa ya Tanzania, lakini anaamini kama atapata nafasi ya kuifundisha timu ya vijana itakuwa ni faraja zaidi kwani atakuwa ametimiza kiu yake ya kufundisha soka na kuinua kiwango cha soka la Afrika ya Mashariki.

Fortune ambaye yuko nchini kwa lengo la kuzindua mashindano ya vijana ya Airtel Raising Stars, alisema anaamini wachezaji wa Ukanda huu wa Sahara wana matatizo yanayofanana na ndiyo sababu ya kushindwa kucheza soka katika ligi kubwa duniani kama England.

"Matatizo ya vijana wengi ni elimu ya soka, wana vipaji, lakini lazima upate elimu kwanza ili uweze kufanya vizuri katika soka,"alisema Fortune.

Fortune alisema tatizo lingine ni kushindwa kutafsiri mikataba mbalimbali ya soka, kushindwa kutambua umuhimu na malengo yao katika soka la kimataifa.

Alisema yeye alifanikiwa kucheza Ulaya kwa sababu aliondoka kwao akiwa na miaka 14 na kujiunga na klabu za huko ambazo zilimtunza kufikia hapo.

"Baada ya kumaliza kozi yangu ya ukocha pamoja na kumaliza kazi nilizopewa na klabu yangu ya Manchester United nitarudi Tanzania rasmi kwa ajili ya kufuatilia soka la Tanzania kwa undani zaidi pamoja na kutafuta vipaji na kufuatilia zoezi la Airtel Rasing Stars linavyoendelea pamoja na kuangalia maendeleo yao baada ya hapa,"alisema Fortune.

Mbali na Uzinduzi huo pia Fortune alitembelea Shule ya Msingi ya Maarifa iliyopo Gongolamboto na kucheza soka na wanafunzi wa shule hiyo huku akikabidhi madawati 30 mipira 40 na jezi jozi tatu

IT'S FRIDAY