Monday, February 6, 2012

GHANA yawasambaratisha waarabu yaifuata MALI nusu fainali

Wachezaji wa Ghana
Ghana "Black Stars"

Andrew Ayew,Johnson Ayew na wachezaji wengine wakishangilia goli lililopeleka msiba Tunisia

Ghana siku ya Jumapili ilifuzu kuingia nusu fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa kuishinda Tunisia magoli 2-1, katika muda wa ziada.
Kipindi cha kawaida cha dakika 90 kilipokwisha, timu hizo zilikuwa sare ya 1-1.
Nahodha wa Black Stars ya Ghana, John Mensah, alifunga bao la kwanza katika mechi hiyo, katika dakika ya tisa, kabla Sabeur Khalifa kuisawazishia Tunisia kabla ya kipindi cha kwanza kumalizika.
Bao la ushindi la Ghana lilifungwa na Andre 'Dede' Ayew.
Ghana 2-1 Tunisia

Katika historia ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, Tunisia haijawahi kuishinda Ghana.
Black Stars sasa wana matumaini ya kuendelea katika mashindano hayo na kupata ubingwa baada ya subira ya miaka 30, na watakutana na Zambia katika nusu fainali itakayochezwa uwanja wa Bata, siku ya Jumatano, tarehe 8 Februari, na ikiwa ni nusu fainali ya kwanza.
Mali na Ivory Coast nao watapambana katika nusu fainali ya pili siku ya Jumatano, katika uwanja wa Libreville.
Mali vs Gabon

Mali ilifuzu kuingia nusu fainali baada ya kuwashinda wenyeji Gabon 5-4 katika kupiga mikwaju ya penalti, baada ya mechi kumalizika kwa sare ya 1-1, na mabao kukosekana hata katika muda wa ziada.
Bao la Eric Mouloungui lilikuwa limewatia matumaini wenyeji Gabon, ambao mwaka huu wamekuwa wakishirikiana na Equatorial Guinea kuandaa mashindano ya mwaka huu.
Lakini kutangulia sio kufika, na Tidiane Diabate aliweza kuisawazishia Mali, zikiwa zimesalia dakika tano tu kabla ya mechi kumalizika.
Kwa kushindwa kufungana katika muda wa ziada, ilikuwa ni pigo kubwa wakati wa mikwaju ya penalti, Pierre-Emerick Aubameyang aliposhindwa kuifungia Gabon bao.
Gabon hawajawahi kufuzu kufika nusu fainali za mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika.
Idhaa ya Kiswahili ya BBC, ikishirikiana na redio washirika, itakutangazia nusu fainali kati ya Mali na Ivory Coast kutoka mjini Libreville, Gabon, katika matangazo maalum ya Ulimwengu wa Soka.
Charles Hilary vile vile atakutangazia mechi ya fainali ya mashindano hayo.

WEBB aibeba Man United kutoa sare na Chelsea

Howard Webb refa alieibeba Man United

Meneja wa Chelsea, Andre Villas-Boas, amelalamika kuhusiana na uamuzi wa Howard Webb, baada ya timu yake ambayo ilikuwa ikiongoza magoli 3-0, hatimaye ilipotoka sare ya magoli 3-3 na Manchester United katika mechi ya Jumapili.
Chelsea, ikichezea uwanja wa nyumbani wa Stamford Bridge, ilionekana kuelekea kupata ushindi, lakini kufuatia uamuzi wa refa Webb, Wayne Rooney aliweza kufunga magoli mawili ya penalti, na mchezo kubadilika.
Chelsea 3-3 Man United

Sare hiyo imeiwezesha Manchester United kupunguza tofauti kati yake na majirani Manchester City, na ambao wanaongoza ligi, kuwa pointi mbili tu kati yao.
"Penalti ya kwanza ilikuwa ni wazi, na hakuna la kusema, lakini ya pili, ni ya kutiliwa shaka kabisa", alielezea Villas-Boas.
"Sijui kama Howard Webb alikuwa katika nafasi muwafaka ya kuweza kuona vyema na kufanya uamuzi, lakini ni jambo la kutoridhisha kwa yeye kutoa penalti hiyo", alilalamika meneja wa Chelsea.
Villas-Boas aliongezea: "Sijui kama Howard alikuwa analipizia jambo fulani ambalo hakulifanya katika nusu ya kwanza, lakini uamuzi wake haukufaa".
Meneja wa Manchester United Sir Alex Ferguson alisisitiza kwamba penalti zote mbili zilikuwa halali, na akielezea kwamba hata walistahili penalti zaidi, baada ya Gary Cahill kugongana na Danny Wellbeck katika kipindi cha kwanza.
"Tungeliweza kupata jumla ya nafasi nne za penalti", alisema.
Katika mchezo wa awali wa Jumapili, Papiss Demba Cisse, aliyesajiliwa na Newcastle, na akicheza mechi yake ya kwanza, aliweza kuifungia timu yake bao, na wakapata ushindi wa magoli 2-1 dhidi ya Aston Villa.
Newcastle sasa imo katika nafasi ya tano katika ligi kuu ya Premier kufuatia ushindi huo.
Cisse alisajiliwa kwa pauni milioni 10.
Mapema mwenzake kutoka Senegal, Demba Ba, alikuwa ameiwezesha timu yake kupata bao la kwanza katika mechi hiyo, lakini Robbie Kean akaisawazishia Villa.