Friday, September 23, 2011

Claudio Ranieri akabidhiwa mikoba ya Gian Piero Gasperini Inter Milan

Kocha wa zamani wa Chelsea Claudio Ranieri ametangazwa kuwa kocha mpya wa Inter Milan kwa mkataba unaokwenda hadi mwaka 2013.
Ranieri
Kocha mpya wa Inter

Tangazo hilo limefuatia kufukuzwa kazi kwa Gian Piero Gasperini siku ya Jumatano asubuhi.
Gasperini alisimamishwa kazi baada ya kufungwa mechi nne na kutoka sare mchezo mmoja katika mechi tano ambazo alikuwa akiongoza kikosi hicho.
Gasperini alikuwa amechukua nafasi ya Leonardo mwezi Juni.
Gasperini
Gasperini

Hii itakuwa kazi ya kwanza kwa Ranieri tangu alipoondoka Roma mwezi Februari kutokana na kupoteza mechi nne mfululizo.
"Claudio Ranieri sasa ni kocha rasmi wa Inter," imesema taarifa ya klabu hiyo siku ya Alhamisi.
Chini ya Gasperini, Inter ilifungwa 3-1 dhidi ya timu iliyopanda daraja msimu huu Novara, siku ya Jumanne, na kupoteza michezo dhidi ya Palermo kwenye ligi kuu, Trabzonspor katika Klabu Bingwa Ulaya, na kwa mahasimu wao AC Milan kwenye mchezo wa kombe la Italia.
Mchezo pekee katika uogozi wa Gasperini uliomalizika bila kufungwa ni sare ya 0-0 dhidi ya Roma wiki iliyopita.
Hata hivyo Ranieri ambaye aliwahi pia kuwa kocha wa Juventus amekuwa akisuasua kushida vikombe. Kombe la mwisho aliloshinda lilikuwa la Italian Cup mwaka 1996 akiwa na Fiorentina, na pia kombe la Hispania akiwa na Valencia miaka mitatu iliyofuatia.

Bob Bradley amrithi Shehata timu ya taifa ya Misri

Kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Marekani, Bob Bradley, Alhamisi ametangazwa kuwa sasa ni kocha mpya wa timu ya taifa ya Firauni ya Misri.
Mkataba wa Bradley utaendelea hadi fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil, kufanyika mwaka 2014.
Bob Bradley
Anachukua ukocha kutoka kwa Hassan Shehata aliyejiuzulu baada ya mfululizo wa matokeo ya kutoridhisha
Atakuwa akipokea mshahara wa dola za Marekani 40,000 kwa mwezi.
Kulikuwa na fununu kwamba Bradley alitazamiwa kuiongoza timu ya Misri ya Firauni, na aliweza kupata mkataba huo baada ya mashauri na chama cha soka cha Misri mjini Cairo.
Anatazamiwa kuitisha mkutano na waandishi wa habari siku ya Jumamosi, ili kuelezea mipango yake, katika kuinyanyua timu hiyo ambayo imekuwa ikifanya vibaya hivi majuzi.
Misri imetwaa ushindi katika awamu tatu za fainali ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, lakini wakati huu imeshindwa kufuzu kushirikishwa katika fainali zijazo kufanyika katika mataifa ya Equatorial Guinea na Gabon mwaka 2012.
"Wachezaji wa Misri ni wazuri mno," alielezea mara tu baada ya kufika Cairo.
"Nchini Marekani tulijitahidi kuwaimarisha wachezaji katika nyanja zote; kiufundi, kimaarifa, miili yao pia, na nadhani ni muhimu kufanya hivyo."
Hisia za mashabiki na vyombo vya habari hazijajitokeza waziwazi kufuatia Bradley kutangazwa kama kocha mpya nchini Misri.
Bradley awali alitazamiwa kuwasili Misri siku ya Jumanne, lakini akacheleweshwa kutokana na matatizo katika kupata ndege.
Chama cha soka cha Misri (EFA), kilikuwa kimefikiria pia kumpa kazi hiyo kocha wa zamani wa Ghana, Milovan Rajevac, lakini hatimaye kikaamua kumwajiri Bradley.
Bradley anachukua wadhifa ulioachwa wazi na Hassan Shehata, ambaye aliamua kujiuzulu kutokana na mfululizo wa matokeo mabaya katika mechi za awali za kufuzu kushirikishwa katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika 2012.
Timu ya Firauni, licha ya kwamba hawana tena nafasi ya kufuzu kwa mashindano hayo, watakuwa ni wenyeji wa timu ya Niger, katika mechi yao ya mwisho ya kufuzu mwezi Oktoba.