Monday, August 22, 2011

Simba kidedea yaua 2-0,Yanga(viti maalum) yachezeshwa kwata na maafande.

Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Vodacom, Yanga(viti maalum), jana walianza vibaya utetezi wao kwa kufungwa bao 1-0 na JKT Ruvu huko Morogoro Uwanja wa Jamhuri lakini Watani zao Simba walianza vyema mno huko Sheikh Amri Abeid baada ya kuichapa Timu mpya kwenye Ligi Kuu JKT Oljoro kwa bao 2-0.
Simba walifunga mabao yao yote kwenye Kipindi cha Kwanza na Straika toka Uganda Emmanuel Okwi ndie aliefunga bao la kwanza kwenye dakika ya 5 na la pili kufungwa na Kiungo kutoka Rwanda Patrick Mafisango dakika ya 15.
Mabingwa hao wa Ngao ya Jamii walichezesha Kikosi kile kle kilichotwaa Ngao ya Jamii Jumatano iliyopita walipowafunga Yanga 2-0 Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.
Kwenye mechi hiyo, Mchezaji wa Simba Uhuru Selemani alirudi tena dimbani baada ya zaidi ya Mwaka mmoja kuwa nje akiuguza goti ambalo ilibidi apelekwe India kufanyiwa upasuaji.
Uhuru aliingizwa dakika ya 60 kumbadili Salum Machaku.
Huko Uwanja wa Jamhuri, Morogoro, Mabingwa Yanga walifungwa bao 1-0 na JKT Ruvu kwa bao la penati iliyopigwa na Kessy Mapande baada ya Beki wa Yanga Chacha Marwa kumfyeka Amosi Mgisa.
Kwa ujumla, Yanga walionekana goigoi katika mechi nzima.

VODACOM MISS TANZANIA 2011 YAPAMBA MOTO



Warembo wanaoshiriki shindano la Vodacom Miss Tanzania 2011 wakiwa katika picha ya pamoja. Warembo hawa wamerejea jana katika jumba la Vodacom baada ya kumaliza ziara yao ya siku kumi kutembelea mbuga za wanyama za Mikumi, mji wa Monduli, Ngongoro, Tarangire, Arusha mjini kuhamasisha utalii wa ndani nchini pamoja na kufanya shughuli mbalimbali za kijamii wakiwa katika ziara hiyo.

Wenger sajili haraka-Graham

Meneja wa zamani wa Arsenal George Graham, amesema Arsene Wenger anahitaji kuwa na wachezaji wenye mbinu tofauti iwapo anahitaji tena kushinda vikombe.
Wenger akitoka uwanjani baada ya kufungwa na Liverpool
Wenger akitoka uwanjani baada ya kufungwa na Liverpool

Akizungumza katika kipindi cha michezo ya wiki cha Radio 5, Graham amesema Arsenal itakuwa na kibarua kigumu iwapo itahitaji kumaliza katika nafasi nne za juu katika msimamo wa ligi msimu huu.
"Wanaonekana hawako imara. Kila mmoja alikuwa anafahamu Fabregas ataondoka," alisema.
"Siamini kama hawajapata mtu wa kuziba nafasi ya Fabregas. Wanahitaji wachezaji wenye uzoefu kuwasaidia vijana hodari walionao."
Graham amempongeza Wenger kwa kushinda mataji mara tatu, lakini akasema kikosi cha sasa ni tofauti kabisa na kile kilichokuwepo msimu wa 2003-04 ambacho hakikupoteza mchezo hata mmoja katika mechi zote 38 za Ligi Kuu ya Soka.
Wenger anazo pesa alizouzia wachezaji akina Cesc Fabregas aliyejiunga na Barcelona, pamoja na Gael Clichy aliyehamia Manchester City na Emmanuel Eboue aliyekwenda Galatasaray.
Mipango ya Samir Nasri kuhamia Manchester City bado ipo hai, licha ya taarifa za mazungumzo kukwama baina ya vilabu hiyvyo viwili.
Graham aliendelea kueleza, "Nadhani wanahitaji wachezaji wengine watatu katika kikosi cha sasa.
Alimtafadhalisha Wenger: "Tafadhali toa pesa. Ninachoona wanahitaji mlinzi wa kati mwengine, kiungo mwenye uzoefu na bado wanahitaji mshambuliaji mwenye kukaribia au kuzidi uchezaji wa Thierry Henry.
Arsenal msimu huu wameweza kumnunua mshambuliaji Gervinho kutoka Lille, na chipukizi wa kutumainiwa Joel Campbell, Carl Jenkinson na Alex Oxlade-Chamberlain.

Man City yachanja mbuga.

Bao la kusawazisha dakika za nyonge kipindi cha pili lililofungwa na Kenwyne Jones liliinyima ushindi Norwich iliyokuwa ikicheza pungufu ya mchezaji mmoja katika mechi ya kwanza ya Ligi Kuu ya England kuchezwa uwanja wa Norwich wa Carrow Road kwa kipindi cha miaka sita iliyopita.
Kenwyne Jones
Kenwyne Jones

Norwich walikuwa wa kwanza kupata bao katika dakika ya 37 baada ya mpira wa kichwa uliopigwa na Ritchie De Laet kumpita mlinda mlango wa Stoke Asmir Begovic.
Leon Barnett alitolewa nje kwa kadi nyekundu baada ya kumfanyia rafu Jon Walters, rafu iliyosababisha kupigwa mkwaju wa penalti uliookolewa na mlinda mlango John Ruddy.
Lakini Jones, aliyesajiliwa kutoka Sunderland mwaka 2010, alivunja matumaini ya Norwich kwa kupachika bao la kichwa tena katika dakika za majeruhi.
Nayo Wolves imeendelea kumajiimafrisha na kupata ushindi wa pili mfululizo msimu huu baada ya kuilaza Fulham mabao 2-0.
Kevin Doyle akichanja mbuga
Kevin Doyle akichanja mbuga

Bao la kwanza la Wolves lilipachikwa katika dakika ya 42 baada ya kazi nzuri ya Kevin Doyle kwa mkwaju maridadi kabla ya Matt Jarvis kumalizia kazi na kufunga bao la pili dakika moja kabla ya mapumziko.
Matokeo hayo yanaifanya Wolves kushikilia nafasi ya pili nyuma ya Manchester City wote wakiwa na pointi sita.
Manchester City ikicheza mtindo wa kushambulia kwa kasi msimu huu ilifanikiwa kuilaza Bolton mabao 3-2 nyumbani kwao katika mechi iliyokuwa ya kusisimua.
Edin Dzeko
Edin Dzeko

David Silva aliipatia City bao la kwanza kwa mkwaju wa pembeni mwa sanduku la hatari la Bolton wakati mlinda mlango Jussi Jaaskelainen akiwa hajajiandaa na kupishana na mpira ukiwa unaelekea wavuni.
Gareth Barry baadae akaachia mkwaju wa mbali na kuipatia City bao la pili kabla ya Ivan Klasnic kufufua matumaini ya Bolton kwa kuandika bao la kwanza kutokana na pande la pembeni kutoka kwa Martin Petrov.
Manchester City walionekana kuendelea kudhibiti mchezo baada ya Edin Dzeko kuanchia mkwaju katika dakika ya pili tu ya kipindi cha pili akiwa ndani ya sanduku la lango la Bolton na kuandika bao la tatu na licha ya Kevin Davies kuifungia Bolton bao la pili kwa kichwa, bado City waliendelea kumiliki mchezo zaidi.
Sergio Aguero wa Manchester City angeweza kufunga mabao kwa urahisi mara mbili baada ya kupatiwa mpira na Dzeko, lakini alipiga mkwaju uliopaa na baadae kichwa alichopiga mpira ukatoka nje sentimita chache ya lango la Bolton.
Kwa ujumla lilikuwa pambano la kuvutia sana huku wachezaji wa Manchester City wakionana kwa pasi murua na kufanikiwa kuipenya ngome ya Bolton mara kwa mara.
Carlos Tevez aliyekuwa mchezaji wa akiba hatimaye aliingia kuchukua nafasi ya Aguero, lakini namna Dzeko, Aguero na Silva walivyokuwa wakionana kunampatia meneja wa City Roberto Mancini matumaini ya kufanya vizuri kwa timu yake msimu huu, hata kama Tevez ataondoka au la.

Arsenal mbovumbovu yagaragazwa na Liverpool

Liverpool dakika za mwisho iliweza kupata mabao mawili ya haraka haraka na kupata ushindi wa kwanza kwenye uwanja wa Arsenal kwa miaka 11 iliyopita, hali ilnayozidi kumtia matatani meneja wa Arsenal, Arsene Wenger.
Suarez na Meireles wakishangilia bao la pili
Suarez na Meireles wakishangilia bao la pili

Arsenal - ikimchezesha Samir Nasri wakati huu mipango ya uhamisho wake kwenda Manchester City ikiwa imesita, iliweza kuwabana Liverpool hadi kiungo wao wa kutumainiwa Emmanuel Frimpong alipotolewa nje kwa kadi nyekundu zikiwa zimesalia dakika 20 kabla mchezo kumalizika.
Meneja wa Liverpool Kenny Dalglish haraka akamuingiza Luis Suarez na Raul Meireles uamuzi ulioonekana kuwa wa maana na wachezaji hao wawili walikuwemo katika mchakato wa kupatikana mabao hayo mawili.
Walishirikiana vizuri langoni mwa Arsenal hadi kijana chipukizi Ignasi Miquel, aliyechukua nafasi ya Laurent Koscielny aliyeumia, aliokoa mpira ambao ulimgonga Aaron Ramsey na kujaa wavuni na muda mfupi baadae Suarez alifunga bao la pili rahisi baada ya kupata pasi kutoka kwa Meireles katika sekunde za mwisho na kukamilisha ushindi wa kwanza wa Liverpool msimu huu.
Nayo klabu ya Newcastle iliendelea kufanya vizuri na kupata ushindi wa ugenini wa bao 1-0 dhidi ya Sunderland kwa bao lililofungwa na Ryan Taylor.
Alan Pardew meneja wa Newcastle
Alan Pardew meneja wa Newcastle

Wenyeji Sunderland walimiliki mpira kwa kiwango kikubwa kipindi cha kwanza, lakini Joey Barton wa Newcastle alikosa bao baada ya mpira wake wa kichwa alioupiga kumgonga Sebastian Larsson mkononi.
Stephane Sessegnon na Asamoah Gyan walikosa nafasi za kuipatia mabao Sunderland, wakati beki wao Phil Bardsley alitolewa nje kwa kadi ya pili ya manjano.
Ushindi huo wa Newcastle ina maana Newcastle imepoteza mechi moja tu kati katika michezo 13 iliyopita dhidi ya wapinzani wao hao wa jadi na ulikuwa ni ushindi wa kwanza kwa meneja Pardew tangu alipochukua hatamu za kuiongoza msimu uliopita.
Nayo Queens Park Rangers ama QPR wamefanikiwa kupata ushindi wao wa kwanza wa Ligi Kuu ya Soka ya England tangu mwaka 1996 baada ya mkongwe Tommy Smith kufunga bao lililoihakikishia ushindi huo wa kwanza wa ugenini dhidi ya Everton.
Adel Taraabt
Adel Taraabt

Eberton inayokabiliwa na matatizo ya fedha imekuwa ni mechi yao ya kwanza ya ligi kupoteza msimu huu.
Mabao yaliyofungwa na Gabriel Agbonlahor, Emile Heskey na Darren Bent yameipa ushindi Aston Villa katika mechi ya kwanza uwanja wa nyumbani wa Ligi kwa meneja Alex McLeish katika uwanja wa Villa Park.
Aston Villa na Blackburn
Aston Villa na Blackburn

Villa ilipata bao la kuongoza lililofungwa na Agbonlahor. Lilikuwa ni bao murua sana kwa mkwaju uliochongwa kwa ustadi na kujaa wavuni.
Heskey alifunga bao la pili kwa mkwaju wa chini chini kwa mkwaju wa yadi 20, lakini Morten Gamst Pedersen alifanikiwa kuifungia bao la kwanza Blackburn baada ya krosi ya Hoilett.
Lakini Bent aliihakikishia ushindi Aston Villa kwa bao la tatu rahisi baada ya mkwaju karibu na lango na kumpita mlinda mlango Paul Robinson.
Swansea City nayo ilifanikiwa kupata pointi ya kwanza katika kwanza Ligi Kuu ya England lakini mkwaju wa penalti waliopatiwa Wigan katika kipindi cha pili uliokolewa na mlinda mlango wa Swansea Michel Vorm na kuinyima ushindi Wigan.
Mlinda mlango huyo mpya aliyesajiliwa msimu huu, Vorm aliokoa mkwaju wa chini chini wa Ben Watson baada ya Jordi Gomez kuangushwa na Ashley Williams.

Mutharika afukuza kazi mawaziri wote

Rais wa Malawi, Bingu wa Mutharika, amelifuta kazi baraza lake lote la mawaziri baada ya majuma kadha ya maandamano ya ghasia, ambapo watu karibu 20 wamekufa.
Maandamano ya Malawi

Bwana Mutharika sasa ameshika wizara zote 42; na hakutoa sababu ya kufanya hivo.
Mataifa kadha ya magharibi, yamesimamisha msaada kwa Malawi baada ya waandamanaji kuuwawa mwezi uliopita, ambao wakilalamika juu ya kupanda kwa gharama za maisha na kama walivosema, serikali mbovu.